Jumapili, 22 Desemba 2013




MAMBO YA KUTAFAKARI KATIKA KIPINDI HIKI CHA CHRISTMAS
http://sanga.files.wordpress.com/2011/12/tree.jpg?w=540
Heri ya Christmas mpenzi msomaji!
Mathayo 1:21 ‘Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina Yesu, maana, yeye ndiye atayewaokoa watu wake na dhambi zao’.
Hakika hii ni sherehe ya ajabu na ya kipekee sana maishani kwetu. Kila mwaka ifikapo Desemba 25, Wakristo duniani kote huadhimisha sherehe ya kuzaliwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo. Naam kuna mambo mengi ambayo hufanyika katika siku hii au katika kipindi cha maadhimisho ya siku kuu hii. Wapo wanaojua maana ya siku hii na wapo ambao wameigeuza siku hii kuwa chukizo mbele za Mungu kutokana  na matendo yao.
Hivyo tunapoadhimisha sherehe hii katika mwaka huu, yafuatayo ni mambo ambayo tumeona ni vema tukakumbushana nayo ni;
  • Mwokozi amezaliwa
Mstari wa 21 wa kitabu cha Mathayo unatueleza kusudi la kuja kwake Bwana wetu kuwa ni kuwaokoa watu wake na dhambi zao. Naam ni upendo wa pekee sana kwa Bwana Yesu kuacha heshima na utukufu mbinguni na aje azaliwe, afe na kufufuka ili tupate waokovu. Kwa sababu hiyo kama bado hujaokoka ni vema ukafanya maamuzi ya kuokoka. Haukuwa uamuzi rahisi kwa Yesu kuacha heshima na enzi mbinguni aje kwa ajili yetu. Na wewe uliyeokoka usiendelee kuishi maisha ya dhambi kama asiyemjua Mungu.
  • Boresha uhusiano wako na Roho Mtakatifu
Biblia inasema ‘Kuzaliwa kwake Yesu kulikuwa hivi, Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana na mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu’ (Matahyo 1:17)
Mimba ya Bwana wetu ndani ya Mariamu ilikuwa ni kwa uwezo wa Roho Mtakatifu. Nasi tunajua ya kwamba, Roho Mtakatifu ni Mungu, na kwa sasa yeye ndiye ambaye yupo duniani analiandaa kanisa la Bwana na kuhakikisha kusudi la Mungu kupitia ‘mtu’ linafanikiwa. Naam ni muhimu sana kila aliye wa Kristo kuhakikisha kwamba mahusiano yake na Roho Mtakatifu yanakuwa mazuri daima. Naam tumia kipindi hiki kumshukuru Mungu kwa siku hii na kujenga msingi mzuri wa mahusiano na Roho Mtakatifu kuanzia sasa na kuendelea.
  • ‘Christmas’ siyo siku ya kufanya uovu
Ni vema watu wote wakatambua kwamba siku hii siyo siku ya kufanya kila namna ya uchafu na dhambi ambazo wanadamu wamezoea kufanya katika siku hii. Ni vema siku hii ikaheshimika sana, maana ndiyo siku ambayo dunia ilipokea mwokozi wa ulimwengu. Naam siku ambayo ufumbuzi wa dhambi ulikuja kwa wanadamu duniani. Shetani amekuwa akijaribu kuharibu sifa/ picha (image) ya siku hii, kwa kuwafanya wanadamu wapange kufanya kila namna ya machikizo mbele za Mungu wetu. Ole kwao wafanyao hayo, naam tulio wa Kristo Yesu tunajua maana ya siku hii na tunaona fahari kwa ajili ya siku hii, utukuzwe Baba kumtoa mwanao, utukuzwe mwana kwa kukubali kuja ili tupate kuwa warithi wa ufalme wako tungali dunani na kisha uzima wa milele.
  • Fanya tathmini ya wokovu wako
Kwa kawaida wanadamu hufanya tathimini ya mambo mbalimbali katika maisha yao. Ni wachache sana ambao hufanya tathmini juu ya maisha yao ya wokovu ndani ya Kristo. Katika mwaka 2013, je umekuwa Balozi wa kweli wa Kristo katika nyumba, ofisi, mji au Taifa lako na kwa wale wanaokuzunguka kila siku? vipi kuhusu uaminifu, je umekuwa muaminifu kwa kiasi gani mbele za Mungu, je unaweza kusema umeishi maisha ya ushuhuda katika Kristo Yesu nk.
Vipi kuhusu mahusiano yako na wenzako, je kuna amani, vipi kuhusu zaka na dhabihu? Kwa kifupi katika vigezo vyote vya wokovu alama zako zikoje, ingekuwa unajiwekea alama katika mia moja ungejiwekea ngapi? na Bwana naye angekuwekea ngapi? Naam pale unapoona hukufanya vema, omba toba na kuomba nguvu mpya ya kukusaidia kipindi kinachofuata.                           MIMI NA FAMILIA YANGU TUNAWATAKIA KHERI YA  CHRISTMASS NA MWAKA MPYA.
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 maoni:

Chapisha Maoni

Item Reviewed: Description: Rating: 5 Reviewed By: Unknown
Scroll to Top