Jumanne, 29 Oktoba 2013






SIRI nzito imefichuka kuwa miongoni mwa walioficha mabilioni ya fedha nchini Uswisi yumo mmoja wa wanasiasa maarufu anayetajwa kuwa anataka kuwania urais mwaka 2015.   Sakata la mabilioni ya fedha za Tanzania kufichwa nchini Uswisi liliibuliwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema), ambapo kwa sasa yupo nchini humo kwa ajili ya kufuatilia kwa kina fedha hizo na waliozificha.   Hata hivyo, kutokana na uzito wa suala hilo, Kamati

Maalumu ya Bunge imepewa jukumu la kufuatilia fedha hizo ambazo baada ya kubainika kufichwa ziliibua mjadala mkubwa nchini huku wanasiasa kadhaa wakitaka walioficha watajwe hadharani na ikiwezekana zitaifishwe.   Taarifa ambazo Jambo Leo imezipata zinaeleza kuwa miongoni mwa majina ya watu ambao wanadaiwa kuweka fedha hizo yumo mwanasiasa maarufu anayetajwa kuwania urais (jina tunalo).   “Tuna taarifa za uhakika kuwa mmoja wa
wanasiasa anayetajwa kutaka kuwania urais mwaka 2015 naye anahusishwa kuwa ameficha fedha 

Uswisi. Tunaamini Zitto atakuja na ukweli maana analifuatilia kwa karibu,” kilidokeza chanzo chetu cha habari.

Hata hivyo, Zitto wakati anazungumzia suala hilo kabla ya kuondoka kwenda Uswisi alisema  Watanzania watafahamu ukweli kuhusu fedha hizo kuanzia walioficha majina na akaunti zao.   Akitoa maoni yake kuhusu mabilioni ya fedha za Tanzania kufichwa nchini Uswisi, Mbunge wa Jimbo la Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), alisema ni vema ikafahamika mtu au mfanyabiashara kuweka fedha nje ya nchi yake si kosa.   Alifafanua kuwa kosa linaweza kujitokeza iwapo katika kuweka fedha hizo taratibu za Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ambayo huidhinisha suala hilo haukufuatwa. “Mfanyabiashara au mtu yeyote anaweza kuweka fedha nje kama amekubaliwa na taratibu husika za BoT.

“Kama amekubaliwa hakuna pingamizi na atakuwa huru kuweka fedha zake, katika hilo hawezi kupata msukosuko kwani kila kipengele ametimiza kikiwemo cha kukatwa kodi halali ya fedha hizo,” alisema.
Hata hivyo, alisema fedha hizo ambazo zinadaiwa kufichwa nchini Uswisi zinaweza kuwa na mambo makubwa mawili, moja zimefuata utaratibu au kutofuata taratibu za BoT.
“Inawezeka kuna ajenda nyingine ya fedha hizo kufichwa kwa sababu tu ya kutaka kukwepa kulipa kodi halali na kujipatia fedha kwa njia isiyokuwa sahihi,” alisisitiza.

Pia alisema inawezekana sababu nyingine ya kuficha  fedha hizo ni kwamba zimepatikana kwa njia haramu ikiwemo ya biashara ya dawa za kulevya au kamisheni iliyotokana na njia isiyo halali na kufanya wenye fedha hizo kuzifichwa nje ya Tanzania.

Alipoulizwa kuhusu kuwepo kwa jina la mwanasiasa anayetaka kuwania urais mwaka 2015 kuwa anadaiwa kuweka fedha Uswis akishirikiana na wenzake, alijibu kuwa katika maisha yake haamini habari za kusikia bali anataka habari ambazo zimethibitishwa.
“Niwaombe Watanzania wenzangu kuwa hakuna sababu ya kuishi kwa kusikia habari za fununu, ni vema mkafanyakazi kwa taarifa za uthibitisho. Siku hizi imekuwa ni mambo ya kawaida watu kushutumiana na kuchafuana kwa kutaja majina ya watu bila ushahidi.
“Hili si jambo nzuri tunapaswa kubadilika. Ni dhambi hata kwa Mwenyezi Mungu kumshutumu mtu bila sababu,” alisema.

Kuhusu sakata hilo, alisema Bunge liliunda kamati ya kuchunguza suala hilo na bado inamalizia kazi hiyo na kwamba ripoti yake itakabidhiwa katika vikao vijavyo vya Bunge, hivyo ni vema Watanzania wakawa na subira na si kuanza kutajana majina kwa lengo la kuchafuana.
“Nimefurahishwa na juhudi zinazofanywa na Zitto kuhusu ya jambo hilo na ninaamini kwa vile ni miongoni mwa watu wanaolichunguza atakuja na majina ya watu waliotorosha fedha hizo nje ya nchi na kuwataka Watanzania wasubiri,” alisema.

Pia alisema kama ni kweli anayetajwa ni mgombea urais mtarajiwa basi sifa zake zitaishia hapo kwani hata baba wa taifa aliwahi kusema mtu anayetumia fedha kuingia Ikulu atakuwa amezipata wapi na atazirudishaje.   Mwenyekiti wa Demokratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila alisema haamini kama Zitto anaweza kuwa na majibu sahihi maana hao hao ambao wameficha fedha ana maslahi nao kisiasa.

“Pamoja na porojo na propaganda zinazotolewa na Zitto jibu atakalokuja nalo baada ya kutoka Uswisi halitakuwa na mshiko kutokana na yeye kuwa na maslahi tofauti na watu wanavyofikiri,” alisema Mtikila.
Hata hivyo, Zitto amekuwa akizungumzia msimamo wake kuwa atahakikisha analisimamia na 

Watanzania watapata ukweli na kamwe hatayumbishwa na mtu yeyote katika suala hilo.   Kabla ya kuondoka mwishoni mwa wiki iliyopita kwenda Uswisi, Zitto aliwataka Watanzania wamuamini kwani anakwenda kutafuta ukweli na wote ambao watakaohusika majina yao atayaanika hadharani.
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 maoni:

Chapisha Maoni

Item Reviewed: Description: Rating: 5 Reviewed By: Unknown
Scroll to Top