Jumatano, 23 Oktoba 2013

Madogo wa Simba walioiua Yanga


 
YANGA itajutia sare ya mabao 3-3 dhidi ya Simba, lakini ukweli halisi ni kwamba, viungo vijana wa Wekundu hao wa Msimbazi, Said Ndemla na William Lucian ‘Gallas’ ndiyo waliiamsha Simba ikasawazisha mabao yote matatu.
Gallas na Ndemla wote kwa pamoja waliingia dakika ya 46 kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Abdulhalim Humoud na Haroun Chanongo waliokuwa wameanza kipindi cha kwanza.
Wachezaji hao ambao wanachipukia kwenye Ligi Kuu Bara na hawana uzoefu na mechi kubwa kama hiyo licha ya msimu uliopita kutumiwa kwenye baadhi ya mechi na kocha Mfaransa Patrick Liewig.
Jumapili iliyopita, Simba walishikika kipindi cha kwanza, wakafungwa mabao matatu ya haraka haraka lakini walipoingia vijana hao hawakufanya makosa, waliibadilisha timu kabisa.
Makosa ya awali yaliyotokana na safu ya kiungo  iliyokuwa na Humoud ambaye alicheza kiungo mshambuliaji mbele ya Jonas Mkude aliyekuwa kiungo mkabaji hayakujitokeza tena, badala yake Simba ikashika usukani na mpira ukachezwa Msimbazi.
Ndemla
Ndemla ambaye anacheza kwa mara ya kwanza mechi ngumu kama hiyo amesema: “Ni mara ya kwanza kucheza mechi ngumu kama hii, lakini kwa sababu niliusoma mchezo kabla sijaingia, ikawa rahisi kwangu. Nikaingia uwanjani na matumaini na sikuhofu kitu na zaidi baada ya kuona benchi la ufundi linaniamini.”
Alikiri kuwa kabla ya kuingia yeye na Gallas  aliona safu ya kiungo chao kilikuwa kimepwaya.
“Niliona Athuman Idd ‘Chuji’ na Frank Domayo ndiyo kizuizi kwetu, wao ndiyo walipandisha sana mashambulizi na kuwapa nafasi washambuliaji wao watushambulie kwa urahisi na nilipoingia nilipambana nao, namshukuru Mungu mambo yalienda vizuri,”anafafanua Ndemla aliyeweka wazi anajisikia mwenye furaha kubwa.
Ndemla mwenye miaka 19, sifa yake kubwa anajua kubadilisha mchezo anapotokea benchi, ana akili ya mpira na sugu anaweza kuingia mahali popote kwenye ugumu.
Simba imempandisha, Ndemla kutoka kikosi chao cha timu ya vijana na kumpa majukumu hayo lakini anapata ugumu kuonekana zaidi kutokana na ushindani wa namba uliopo kwa sababu Simba ina viungo wengi kama, Gallas, Abdallah Seseme, Mkude, Ramadhani Chombo ‘Redondo’, Humoud na Kiemba ingawa ametamka kuwa ana uwezo wa kucheza namba nyingine na kumudu vizuri kama winga ya kulia na namba 10.
“Simba ni timu kubwa yenye ushindani wa juu hasa nafasi ya kiungo ina wachezaji wengi, hiyo ndiyo changamoto kwangu inayonifanya nijitume kwa nguvu zote kuhakikisha napata nafasi kikosi cha kwanza,”anaeleza Ndemla anayeipenda klabu ya Chelsea ya England.
 



  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 maoni:

Chapisha Maoni

Item Reviewed: Description: Rating: 5 Reviewed By: Unknown
Scroll to Top